Archive for January, 2007

Tunapalilia Upumbavu?

“Hapa duniani wale wanaopenda kunyoosha mistari ndio wanaokumbana na matatizo zaidi, wewe pinda tu mistari kisha utaona mambo yanavyokunyookea” – aliyenukuliwa anahifadhiwa.

Naandika makala hii takriban dakika 48 toka nitoke katika chumba cha mtihani nilipokuwa nafanya mitihani yangu ya kumaliza semister ya kwanza kwa kozi ninayosomea ya sheria. Nimetoka kufanya mtihani wa CL (Communication Skills), baada ya ule niliofanya jana wa DS (Developmental Studies).

Naikumbuka nukuu niliyoanza nayo hapo juu baada ya kushuhudia yote yaliyojiri katika siku hizi mbili za kufanya mitihani niliyokwishaitaja na wakati naikumbuka pia najiuliza hivi hayo yaliyojiri katika chumba cha mtihani ni kwa faida ya nani hasa? Ni kwa faida yetu tuliokuwa katika mitihani hiyo au kwa faifa ya nani hasa?

Muda mfupi baada ya kutoka katika chumba cha mtihani (nikiwa wa kwanza), alitoka mwanafunzi mwenzangu mmoja na tambio kadhaa wa kadha kuhusu “atakavyopasua” (akimaanisha kufaulu) mitihani hiyo. Nilimwangalia nikamtupia swali kwamba “Je, katika kupasua huko ni kwa asilimia ngapi atakuwa ametumia uwezo wake na kwa kiasi gani atakuwa alisaidiwa?”

Nilimtupia swali hilo kutokana na pilika pilika nilizokuwa nazishuhudia akizifanya yeye na baadhi ya wanafunzi wenzangu katika kupasiana vijikaratasi sijui niviite vya majibu au vya nini maana sina uhakika kama kweli yalikuwa majibu. Ingawa inawezekana kila mmoja akawa na mtazamo wake kuhusu hili, lakini nitakiri kuwa kuna wakati pilika pilika hizo zilikuwa zikinikera kwa namna moja ama nyingine. Zilikuwa zinanikera kwasababu sikujua kuwa zilikuwa zinafanyika kwa faida ya nani na kwa ajili ya kumkomoa nani hasa.

Asilimia kubwa ya ninaosoma nao ni watu wazima tu, wenye familia zao, wenye watoto wao na ambao wanawasomesha watoto hao. Inawezekana kuwa wapo kati yao hawana utamaduni wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao lakini ukweli unabakia pale pale kuwa wote kwa ujumla wanataka kila mwisho wa mhula mtoto awe amefanya vyema katika mitihani yake.

Kwa mzazi wa aina hii anapoamua kuingia darasani, akajilipia ada yeye mwenyewe kwa lengo la kujiendeleza kielimu, ni wazi kuwa katika kiwango chake haitarajiwi awe na akili sawa na za mtoto wake. Ni wazi kuwa anatakiwa kuhakikisha kuwa kila aina ya senti aliyoitumbukiza katika kujisomesha inampa uchungu wa kuhakikisha kuwa inambadilisha kimawazo, kifikra na kimtazamo. Sasa hapa ndipo ninapojiuliza hivi hizo pilika pilika kweli zinamwelekeo wa kutupeleka huko?

Naam, ni wazi kabisa kuwa mzazi wa namna hii sio tu kuwa anazidi kujidunisha zaidi badala ya kujielimisha zaidi, na haitarajiwi kuwa mzazi wa namna hii atasimama kidete kuhakikisha kuwa mtoto wake anakuwa na utaratibu mzuri wa kumwezesha kufaulu mitihani yake. Ndio!! Kama mzazi unakosa kujua kuwa wajibu wako katika kujiendeleza ni kuhakikisha kuwa unatumia uwezo wako kwa kiwango cha hali ya juu, ni vipi utajali kuwa mwanao amefaulu ama kwa kuhonga au kwa kuibia majibu kwa mwenzake?

Na katika hali kama hii tunajenga jamii ya namna gani hasa? Ni wazi kabisa kuwa moja kati ya mambo ambayo yamekuwa yakikwamisha kuendelea kwa uchumi wa taifa letu ni pamoja na kiwango duni cha elimu tulicho nacho. Ni wananchi ambao wanalalamikia hali hii, lakini sasa ni wananchi hao hao ambao hawafanyi juhudi za kuhakikisha kuwa kiwango hicho kinaboreka zaidi kwa kila mmoja kuhakikisha anatumia kikamilifu akili yake. Tunamlalamikia nani hasa ambaye atatukomboa katika hili?

Wengi wetu tumekuwa ama tukisoma kwa ajili ya vyeti au kwa ajili ya kupandishwa cheo kazini, lakini badi hata waliofanya hivyo hawajaweza kuwa na ufanisi wa kutosha katika majukumu yao, yawe ya kiserikali au ya kwenye mashirika binafsi. Usomaji huu kwa ajili ya vyeti na kupandishwa cheop ndio ambao umekuwa ukidumaza elimu yetu. Ndio umekuwa ukizalisha kizazi cha watu wasiokuwa na uchungu na maendeleo, kwasababu kwao kila jambo ni rahisi sana kama kuibia majibu ya mitihani.

Na hata mifumo yetu ya ajira imekuwa ya namna hiyo hiyo na huenda ndio maana hata usomaji umekuwa wa uelekeo huu. Ajira zinazotolewa kwa kuangalia wingi wa vyeti ni ajira zisizokuwa na mwelekeo wa kulikomboa taifa hili katika umasikini. Ni ajira ambazo zinawafanya watu wasiokuwa na sifa kukaa maofisini na kuishia kuitisha makongamano, warsha, semina, mikutano nk, wakishania kuwa huko ndio kupambana na umasikini.

Kwakweli sijui wa kumlaumu atakuwa nani ingawa kwa asilimia kubwa sana naamini ni kwetu sisi wenyewe, sababu tungali tunaelea katika kina kirefu cha upumbavu badala ya ujinga. Tumejijengea utamaduni wa kuwa kila kitu ni rahisi sana kama kukisema tu na ndio maana hatutaki kutumia akili zetu. Tumejidumaza kutokana na mifumo ambayo tuliikuta ambayo kama tukiwa na uchungu kama tunavyoilalamikia kweli tunatakiwa sisi ndio tusimame kidete kuhakikisha kuwa tunaibadilisha hali hiyo.

Mtanisamehe sana ambao mtakuwa mmeguswa na hali hii lakini nimeona niseme maana ni heri kusema kuliko kukaa kimya. Kwanini tusibadilike na kuwa na mtazamo wa kuendelea katika dunia hii ya sasa ambako tunaona kabisa kuwa mambo si marahisi kama ambavyo tulikuwa tunayaona hapo awali? Tunaingie kwenye mitihani tukitarajia kurushiwa majibu na wenzetu kwa faida ya nani hasa?

4 comments January 9, 2007

"Mwana wa Komba" mwenye jicho linalowaona watoto wa Mitaani

Nadhani ndio wale wale wa kule mahali hawa maana jina tu linajieleza (nadhani Ndesanjo unaelewa namaanisha wa wapi). Huyu ni dada yetu Anna Komba a.k.a Mwana wa Komba, ambaye ameamua kujiunga katika mtandao wa Wanablogi wa Kitanzania. Ilikuwa kama utani vile nilikutana naye mtandaoni siku hiyo tukaongea mambo kadhaa akaniomba nimsaidie kufungua blogi nami nikafanya hivyo, nikadhani itamchukua muda kufikiria “Atoke Vipi” lakini kumbe mwenyewe alikuwa kajipanga anasubiri tu aone njia. Dada Anna ambaye blogi yake ameiita Jicho lake Mtaani ameanza kwa kugusia tatizo sugu la watoto wa mitaani, ingawa siamini kama kuna watoto wa mitaani kweli (nitasema siku nyingine). Mtembelee na umkaribishe kwa kubofya hapa.

Add comment January 8, 2007

BENKI ZETU NA SERA KWA WALALAHOI

Katika pita pita yangu mitaani hivi karibuni, nilikuta kikundi cha wananchi ambao walikuwa wakijadili masuala mbalimbali kuhusu hali halisi za kiuchumi walizonazo. Ingawa mjadala huo mwanzoni kabisa sikuwa nimevutika nao kwa kiasi cha kutosha, nilijikuta nikivutiwa nao baada ya mmoja kati ya washiriki wake alipoanza kuzungumzia kuwa Benki ni mmoja kati ya wakombozi wa walalahoi nchini Tanzania.

Hilo pekee halikuwa tatizo, ila jamaa mmoja alipoamua kumpinga mwenzake kuhusu hoja ya benki kuwa mkombozi. Sehemu ya maongezi ilikuwa kama ifuatavyo:-

Mwananchi A: Siku hizi kuna uwezeshwaji mkubwa lakini kiasi kwamba wakijipanga (sijui kwanini anajitenga), hata benki zinakopesha siku hizi.

Mwananchi B: Benki!! Benki hivi unajua maana ya benki wewe? Hizi benki zetu tafsiri yake ni kukusanya fedha za wananchi walio walalahoi kwa kisingizio cha kuwahifadhia na kuwapatia matajiri. Ndio maana unaona hata kasi yenyewe ya ukopeshaji ni kwa walio nacho, wa kawaida (wananchi), unabembelezwa kuweka fedha zako lakini kwenye kukopa masharti kibaaaaaao, sijui hatimiliki, sijui mambo gani tena, yaani ah!!
==========

Naam, hiyo ni sehemu ambayo ilinivuta zaidi, ikanikumbusha wakati fulani nilipokuwa nasafiri kutoka Dar es salaam kwenda Moshi, nilikuwa na jamaa nao walikuwa wakilalamika eti kuna benki ukiweka fedha zako unapata faida ya asilimia mbili tu (2%) na wakati huo huo ukienda kukopa katika benki hiyo utatakiwa kurejesha mkopo huo kwa riba ya asilimia kumi (10%), nane zaidi ya faida ya kuweka fedha zako.

Tukirejea katika ukweli halisi wa maisha tuliyo nayo hivi sasa, watendaji wa ngazi mbalimbali serikalini na hata kwenye chama hiki kilichoshika hatamu (sio utamu?), wamekuwa wakihanikiza juu ya wananchi kukopeshwa, kukopa au kujitafutia mitaji kwa ujumla ili kuweza kujiajiri au kujifanyia kazi zitakazowaletea tija katika kazi zao.

Ni kweli kuwa katika mazingira ya kawaida kabisa, msingi wa kupatia mtaji ni mkopo, na ndio maana hata serikali zetu zinakopa, lakini je, benki zetu nchini zimeshiriki kwa kiasi gani kuhakikisha kuwa wananchi wananufaika nazo? Ukiachilia mbali miaka ya karibuni ambako juhudi za kuunda vyama vya ushirika wa akiba na mikopo zimekuwa zikiongezeka ili kuwafanya wananchi hao kukopesheka, bado mchango wa mabenki yetu hapa nchini katika kuinua hali za wananchi umeendelea kuwa wa chini sana.

Masharti ya kupata mikopo, urasimu katika kushughulikia maombi yaliyowasilishwa, riba inayotakiwa wakati wa kuurejesha, uhakika wa masoko, miundombinu, elimu ya ujasiriamali, mabadiliko ya hali ya hewa na matatizo mengine kadhaa ni miongoni mwa sababu ambazo zimekuwa zikiathiri suala hili kwa kiasi kikubwa.

Sina hakika ikiwa benki zetu zimejikita katika kuhakikisha zinajiimarisha kwa kuwekeza kwa wananchi walio wa kawaida sana, ambapo zitatakiwa kuhakikisha zinashirikiana nazo katika kuboresha miundombinu ya mawasiliano na uchukuzi, masoko na hata pembejeo. Kwa maana hili ni jukumu ambalo hawawezi kulikwepa.

Wadadisi wa masuala ya kibenki na mahusiano ya jamii wamekuwa wakielezea kuwa ukuaji wa benki yoyote ile umekuwa ukitegemea zaidi ukuaji wa hali ya uchumi kwa wananchi walioko karibu nayo, hivyo ni jukumu la benki husika kuhakikisha kuwa inawekeza zaidi katika rasilimali watu. Sijui kwakweli kama hili limefikiwa kwa kiasi gani hapa nchini, lakini midhali bado hali za wanaoyazunguka mabenki yaliyopo hazijaweza kuwa nzuri, huo ni uthibitisho kuwa uwekezaji wa mabenki yetu katika rasilimali watu ni wa kiwango cha chini sana.

Kwa bahati mbaya sana ni kuwa mabenki mengi yameendelea kuishi kwa dhana ya kuwa uimara wao unatokana na wateja wakubwa wachache, na asilimia kubwa ndio uwekezaji wao ulikoelekea. Hili limekuwa likinipa shida kidogo kwasababu ninavyojua mimi ni kuwa kuwekeza kwa wale wengi walio na hali za chini ni sawa na kujijengea kizazi cha wateja wengi katika miaka ijayo. Inamaana hili halionekani au?

Natambua kuwa kunaweza kukawa na maelezo mengi sana katika hili kutoka kwa watu wa kwenye mabenki mbalimbali, na bilashaka ninayapenda sana maelezo haya yaje hapa ili tuweze kuelimishana na kupeana changamoto, lakini kwa namna yoyote ile bado hali ingali inabaki kuwa kasi ya benki zetu hapa nchini katika kujenga kizazi kitakachozifanya ziwe benki kubwa sana ndani na nje ya nchi, iko chini sana na kuwa mbinu zinahitajika katika hili.

Tuwaone hawa walalahoi kama sehemu muhimu sana kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi, ukuaji wa benki hizi na ukuaji wa huduma na ubora wa maisha, kwa kuona namna ambavyo wanaweza kukopeshwa kwa masharti ambayo yanaendana na hadhi zao. Kuweka masharti ambayo ni vigumu kwa wao kuyafikia tayari ndio kunakosababisha uwepo wa dhana ya kuwa zinachukua fedha zao na kisha kuwakopesha wenye nazo.

Unaweka mashartyi kwamfano ya kuwa sijui na hatimiliki ya kiwanja wakati halmashauri zenyewe zinazotakiwa kupima viwanja hivyo zinashindwa kutimiza wajibu wake hadi kurejesha fedha za kazi hiyo serikali kuu, unadhani huyo mwananchi lini atakuwa wa kukopeshwa? Na huko si kumnyima haki yake kwa kosa au udhaifu wa mtu mwingine?

Naomba nikaribishe changamoto mbalimbali kuhusu hali hii na ikiwa watajitokeza wanataaluma ya benki kwa ajili ya kujadili mjadala huu naamiini tutafanikisha wajibu wetu katika kujenga taifa lililo na wananchi wasiolia njaa kila kukicha

Alamsiki.

tukijipanga

Add comment January 3, 2007

HERI YA MWAKA MPYA


Nawatakia wasomaji wangu wote Heri ya Mwaka mpya wa 2007 . Natumaini Mungu atatujaalia sote kwa pamoja uwe mwaka wa matumaini kwetu, na mwaka ambao nyingi kati ya ndoto zetu zitakuwa kweli. HERI YA MWAKA MPYA WA 2007

Add comment January 1, 2007

Next Posts


Bango la Matangazo & Wazo mahususi

Blogi Nyingine

Blogi za Katuni

Blogi za Picha

Malavidavi!

Mapishi

Mavazi & Mitindo

Vyombo vya Habari

wageni

Webu mseto

Blog Stats

 

January 2007
M T W T F S S
« Dec   Feb »
1234567
891011121314
15161718192021
22232425262728
293031  

Archives

Meta

Pages